Loading...

Utafiti: Mbinu mpya yabuniwa kuendeleza ukeketaji wanawake.


Baadhi ya jamii nchini zimebuni mbinu mpya ya kuendeleza mila potofu za ukeketaji wanawake kwa kuwahamisha kutoka nyumbani kwao kuwapeleka maeneo ya mbali ili wanajamii wasitambue kinachoendelea.
 
Utafiti uliofanywa na Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (Tamwa) kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Idadi ya watu Duniani (UNFPA) katika mikoa 12 ya Tanzania Bara na Zanzibar, umebaini kuwa ukeketaji na ndoa za utotoni bado ni tatizo kubwa.
 
Mratibu wa Kitengo cha Usuluhishi Tamwa, Gladness Munuo, alisema kuanzia Januari hadi Oktoba, 2015 katika wilaya ya Kondoa mkoani Dodoma asilimia 39.9 ya wanawake wajawazito walifanyiwa ukeketaji.
 
Alisema wilaya ya Tarime kesi 118 za ubakaji ziliripotiwa mahakamani, Pemba wasichana wadogo 240 walipata mimba mwaka 2015, huku wilaya ya Mkalama wanawake 2,265 ambao walijifungua katika vituo vya matibabu 115, walifanyiwa ukeketaji.
 
Alisema katika Kata ya Msalala wilaya ya Kahama wasichana 605 ambao ni sawa na asilimia 47.47 kati ya 1,150 hawakumaliza shule za sekondari kwa sababu ya ndoa za utotoni, huku katika wilaya ya Bagamoyo wasichana 12 wa shule waliripotiwa kupata mimba ndani ya miezi sita kuanzia Januari hadi Juni, 2015.
 
Munuo alibainisha kuwa katika maeneo ya Tarime, wasichana hupakwa unga usoni ikimaanisha kuwa hawakeketwi teni, lakini ukweli ni kwamba wamewakeketa na kufanya hivyo ni kuficha ukweli.
 
Alisema kwa upande wa ndoa za utotoni, umebaini kuwa ndoa nyingi chanzo kikubwa ni wazazi na ndigu kwa lengo la kupata mahari na wameshiriki kushawishi watoto wafeli mitihani ili iwe sababu ya wao kuolewa.
 
“Utafiti umebaini visababishi sugu vya ukeketaji na ndoa za utotoni ni pamoja na mila, tamaduni na desturi potofu, umaskini uliokithiri, kukosekana kwa uelewa juu ya haki za binadamu, mfumo dume, ukosefu wa sera imara pamoja na sheria dhaifu ambazo utekelezaji wake hauridhishi, ukosefu wa mabweni, wanafunzi kutembea umbali mrefu hadi shuleni na mwamko mdogo wa wazazi juu ya umuhimu wa kuwaelimisha watoto wa kike,” alibainisha.
 
 
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright KAZI YANGU | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top