Loading...

Ummy: Benki ya Wanawake ni jipu bichi.


Wakati Tanzania ikiungana na nchi zingine duniani kuadhimisha Siku ya Wanawake, Waziri  wa  Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amesema Benki ya Wanawake Tanzania (TWB) ni jipu na linatakiwa kutumbuliwa.
Kutokana na tatizo hilo, Ummy amemwagiza Mkurugenzi Mtendaji wa TWB, Margareth Chacha, kutoa maelezo ndani ya siku tatu kwa nini benki hiyo inatoza riba kubwa zaidi ya asilimia 19 kwa mikopo inayotolewa.
 
Waziri huyo alisema juzi akiwa kwenye shughuli ya wanawake wa mkoa wa Dar es Salaam kupitia Vyama vya Kuweka na Kukopa (vikoba) pamoja na Benki ya Posta, wanawake walikuwa wakilalamikia kuhusu tozo kubwa ya riba kwenye benki ya wanawake.
 
“Zama hizi ni za uwazi na ukweli. Nilisikitika sana benki hii inatoa riba zaidi ya asilimia 19. Siwezi kulikubali hili, wanawake wanaishangilia benki nyingine badala ya benki yao. Mkurugenzi (alikuwapo kwenye hafla hiyo) una kazi ya kufanya, siwezi kusimama kutetea benki ya wanawake kwa hali kama hizi,” alisema na kuongeza:
 
“Nitahitaji maelezo ndani ya siku tatu. Hizi ni zama za Magufuli, hakuna kuoneana aibu, kwa nini benki si rafiki kwa wanawake wakati inapewa fedha na serikali. Hili ni jipu tutalitumbua” alisema.
 
Alisema wanawake walikuwa wanaishangilia  Benki ya Posta ambayo riba yake ni asilimia 11 na kuilalamikia yao.
 
Katika hotuba yake iliyosomwa na waziri huyo, Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan, aliagiza Halmashauri zote zihakikishe zinatenga asilimia tano ya mapato yao ya ndani kwa ajili ya Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake.
Alisema wakurugenzi ambao halmashauri zao hazitatekeleza hilo watawawajibisha.
 
Pia alitaka wakurugenzi watenge maeneo maalum ya biashara ikiwa ni pamoja na na kufuta kodi zenye kero kwa wajasiriamali ambao wengi wao ni wanawake.
 
Alisema ripoti ya Mapitio ya Sera ya Biashara za Kati na Ndogo ya mwaka 2013, inaonyesha wanawake wanamiliki asilimia 64 ya biashara hizo, wakati utafiti wa hali ya uchumi wa mwaka 2010 ukionyesha asilimia 23 ya wanawake wana kipato kisichozidi au kulingana na waume zao.
 
Akikazia suala la wakurugenzi, Mwalimu alisema watakaoshindwa kutenga asilimia tano majina yao yatawasilishwa Ikulu.
 
“Mimi na naibu wangu, Dk. (Hamis) Kigwangalah, hatutashindwa kuwawajibisha wakurugenzi wote ambao hawatatenga asilimia tano kwa ajili ya mfuko huu, asiyetenga huyu ni adui wa wanawake, tutampelekea jina kwa Rais Magufuli, usawa wa jinsia utafikiwa kwa kuwaendeleza wanawake kiuchumi na kielimu,” alisema.
 
Aliongeza kuwa: “Tukikaa kimya hii kauli mbiu ya asilimia 50/50 hadi ifikapo 2030 itakuwa kwa wabunge lakini vijijini haitafikiwa.”
 
Ummy alisema katika kufuatilia utekelezaji wa suala hilo, kila robo na  nusu ya mwaka watakuwa wakitoa orodha ya majina ya wakurugenzi wote wanaozembea kufanya hivyo.
 
Alitolea mfano mkoa wa Dar es Salaam ambao unatengewa Sh. bilioni 47 ya bajeti na kusema ile inayoenda kwenye mfuko wa wanawake ni Sh. bilioni 2.3, ambayo ikitekelezwa maisha ya wanawake yatabadilika.
 
“Hatuwezi kusubiri hadi tutumbuliwe. Tutaanza kuwatumbua ninyi ambao hamtekelelezi hili na kuwanyima wanawake ambao ni asilimia 64 ya watu wote wanaofanya biashara ndogo na za kati,” alisema.
 
Pia aliziagiza halmashauri zitenge maeneo maalumu ambayo wanawake watafanya biashara bila kunyanyaswa.
 
Kadhalika, alisema kila miezi mitatu watakuwa wakizitangaza Halmashauri ambazo zimefanya vizuri na vibaya kwenye suala la vifo vya wajawazito.
 
Alisema watalivalia njuga suala hilo kwa sababu lengo la serikali ni kuvipunguza vifo hivyo.
 
Kuhusu ukatili, Ummy alisema vitendo hivyo vipo kwa asilimia 39 nchini ambapo kwa mkoa wa Dar es Salaam vipo kwa asilimia 31.
 
Alisema kwenye upande wa uandikishaji wa darasa la kwanza, wamefanikiwa kwa asilimia 50 lakini changamoto iko sekondari kutokana na mimba za utotoni.
 
Alimpongeza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiki, kwa jitihada aliyoifanya kuhakikisha inajengwa shule ya wasichana ya bweni, ambayo itasaidia kupunguza changamoto hiyo kwa kiasi fulani.
 
Kuhusu likizo za uzazi, aliwataka wanawake ambao wananyanyaswa,   iwe sekta binafsi au ya umma, kutoa taarifa kwake ili mwajiri achukuliwe hatua za kisheria.
 
“Hili ni tatizo ambalo linafanya baadhi ya wasichana kuogopa kubeba mimba kwa kuhofia kufukuzwa. Tuleteeni taarifa tutawafikisha mahakamani,” alisema.
 
Ummy alisema wataungana na Kamishna wa Polisi wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro, kuhakikisha wakati wa ukamataji wa ‘makahaba’, wanaume ambao ndio wateja wao, nao wakamatwe.
 
Akizungumzia ahadi ya Rais Magufuli ya kutoa Sh. milioni 50 kila kijiji, alisema watakahikisha nusu yake zinaelekezwa kuwasaidia wanawake nchini.
 
Pia alisema watapambana na wanaume wanaowapa ujauzito wanafunzi na kukamata wazazi ambao wameshindwa kutimiza wajibu wao wa malezi.
 
Naye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora, Angellah Kairuki, aliwataka watumishi wa umma wanawake kujiendeleza kielemu ili waweze kushika nyadhifa mbalimbali.
 
Katika maadhimisho hayo, Mbunge wa Njombe, Edward Mwalongo, amepewa tuzo baada ya kauli yake Bungeni kuhusu wanafunzi wa kike wanavyokosa masomo kutokana kukosa zana za kujisitiri, pindi wawapo katika hedhi.
 
Wakati huo huo, pamoja na serikali, wadau mbalimbali kupinga vitendo vya kikatili dhidi ya  wanawake hasa watoto wa kike katika jamii, bado imeshindwa kutoa elimu kuhusu mila kandamizi  zinazochangia kukwamisha ndoto zao.
 
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Mwanamke Duniani, mwakilishi wa Mradi wa Vijana  kwa Mabadiliko,  Nehema Nemno, alisema wanaungana na wanawake wengine duniani kuwakumbusha watoto wa kike umuhimu wa matarajio yao ya badaye.
 
Alisema watoto wa kike wanapaswa kuandaliwa kwa kuzitambua haki zao hasa kuhusu afya ya uzazi, madhara ya ukeketaji pamoja na ndoa za utotoni.
 
“Watoto wa kike baadaye atakuwa mama wa watoto, hivyo akielekezwa na kuzifahamu athari na faida ya jambo anaweza kuondokana katika mila kandamizi zinazokwamisha mfumo wa maisha yake kiujumla,”alisema Nemno.
 
Naye mwakilishi kutoka Shirika la Plan International Tanzania (Plan), Emmanuel Mang’ana, alisema mradi huo uko chini ya shirika hilo, ukijulikana kwa jina la Binti Jitambue, na umekusudia kuwalenga vijana wenye umri wa rika la miaka 16 na kuendelea.
 
Mkuu wa shule ya Sekondari ya Jangwani, Mwani Senga, alisema msichana ili kufika malengo yake anatakiwa kusimama kupigania ndoto zake, hivyo licha ya changamoto nyingi kuliandama kundi hilo, bado nguvu kazi ikielekezwa linaweza kuondokana na adha linalokumbana nazo mara kwa mara.
 
CHANZO: NIPASHE

Post a Comment

CodeNirvana
Newer Posts Older Posts
© Copyright KAZI YANGU | Designed By AFROPIXELS MEDIA CO. LTD
Back To Top